Comments


Kocha Mkongwe wa mchezo wa kuogelea apinga uteuzi wa Magdalena katika mashindano ya Olimpiki


Kocha mkongwe wa mchezo wa kuogelea nchini Ferick Kalengela amepinga uteuzi wa muogeleaji wa kike wa Tanzania, Magdalena Moshi kuiwakilisha nchi katika mashindano ya Olimpiki kupitia tiketi ya Nafasi za Upendeleo iliyolewa na waandaaji.

Chama Cha Kuogelea nchini (TSA) kiliwakilisha jina la mchezaji huyo pamoja na muogeleaji wa kiume, Hilal Hemed Hilal kuiwakilisha nchi kwa njia ya tiketi hiyo, lakini Kalengela amesema kumjumuisha Magdalena ni kinyume na matarajio yao hata kama Shirikisho la Mchezo wa kuogelea Duniani (Fina) kuweka vigezo vyake.

Fina iliweka vigezo kuwa waogeleaji walioshiriki mashindano ya kuogelea ya Dunia yaliyofanyika mwaka jana nchini Kazan kuwa ndiyo wanaopaswa kuwepo katika nafasi ya kuiwakilisha nchini kwa nafasi ya upendeleo. Sonia hakuweza kushirki mashindano hayo ambayo Tanzania iliwakilishwa na wachezaji watatu, Hilal, Ammaar Ghadiyali na Magdalena.

Kalengela alisema kuwa vigezo hivyo havipaswi kutumika kwa uteuzi wa waogeleaji wa Tanzania kwani Magdalena mbali ya kuiwakilisha nchi katika mashindano ya Kazan yaliyofanyika kati ya mwezi Julai na Agosti mwaka jana, hajawahi kushiriki mashindano yoyote hapa nchini kuthibitisha ubora wake.
Kocha huyo mkongwe nchini  alisema kuwa muogeleaji nyota wa kike hapa nchini, Sonia Franco Tumiotto ndiye anapaswa kupewa nafasi hiyo hata kama hajashiriki mashindano ya dunia, lakini matokeo yake ya hapa nchini na nje ya nchi yanampa nafasi.

Alifafanua kuwa Magdalena ambaye anasoma na kuishi nchini Australia, hakuweza kufika mashindano ya Taifa ambayo Sonia alikuwa mshindi wa jumla kwa kushinda medali 10 za dhahabu huku akivunja rekodi 10 mbalimbali za taifa.

“Sonia pia ameweza kushinda medali tatu katika mashindano ya kufuzu Olimpiki ya Dubai akiwa mmoja wa waogeleaji wanne wa timu ya Taifa, alishinda medali ya dhahabu moja na shaba mbili, Magdalena hakushiriki katika mashindano hayo, ilikuwa kazi rahisi tu kwa TSA kupendekeza jina la Sonia kwa kutoa sababu za kiufundi ili aweze kupewa nafasi hiyo, ni kweli kuwa Sonia pamoja na kuwa hajashiriki mashindano ya Dunia, lakini kwa sasa ndiye muogeleaji namba moja nchini kwa upande wa wanawake,” alisema Kalengela.

Alisema kuwa hata ukilinganisha matokeo ya Sonia na Magdalena,  utapata jibu kuwa Sonia ni zaidi ya muogeleaji huyo kwa sekunde 1.30 kwa staili ya freestyle mita 50.  “Je  TSA haijaona hili, je kama ingetokea mmoja wa waogeleaji amepata dharura, nafasi hiyo ingepotea? Tuepuke mazoea na sasa tunatakiwa kwenda kwa uhalisia,  kufanya hivi ni kupoteza ushindani wa mchezo na kuwavunja moyo waogeleaji na wadau hasa wazazi,” alisema.
Katibu Mkuu wa Kamati ya Olimpiki Tanzania (TOC) Filbert Bayi alikiri kupokea jina la Magdalena na Hilal na kuweka wazi kuwa kazi ya Kamati ni kupokea na wala si kuchagua.
1
Muogeleaji wa Tanzania Sonia Tumiotto (wa kwanza kushoto) akipokelewa kwa shangwe Katibu Mkuu wa Chama Cha Kuogelea nchini (TSA), Ramadhan Namkoveka na Katibu Mkuu wa klabu yake (Dar Swim Club), Inviolata Itatiro  mara baada ya kuwasili kutoka Dubai alipokwenda kutafuta tiketi ya kufuzu mashindano ya Olimpiki.  Pamoja na kufanya vyema, muogeleaji huyo hajapewa nafasi ya kuiwakilisha nchi kwa njia ya upendeleo kutokana na  kukosa vigezo vya Shirikisho la Mchezo wa Kuogelea Duniani (Fina) ambazo zinawapa nafasi waogelaji wote walishindana mashindano ya Dunia ya Kazan.

“Awali TSA ilileta majina matatu, wanaume wawili na mwanamke mmoja, nikawaandikia barua kuwataka watume majina mawili kwa mujibu wa taratibu, nikaletewa Hilal na Magdalena, siwezi kufanya lolote, hayo ni masuala ya chama  na shirikisho lao, siwezi kuingilia,” alisema Bayi.
Akijibu madai hayo,  Mkurugenzi wa Ufundi wa TSA, Amina Mfaume alikiri kuwa Magdalena hajashiriki mashindano ya mwaka huu ya Taifa yaliyofanyika kwenye bwawa la Hopac kutokana na kukabiliwa na mitihani, lakini uteuzi wake umetokana na majina yaliyoletwa na Fina.
Amina alisema kuwa  hawahampendelea Magdalena katika uteuzi huo kwani vigezo vya Fina ndivyo vimempa nafasi Magdalena na wao hawawezi kwenda kinyume.
 “Tunafuatilia maendeleo Magdalena ya huko Australia kupitia mwalimu wake, hata Sonia ambaye tupo Uingereza naye tunafuatilia maendeleo yake, hivyo hakuna wasiwasi wa ushiriki wa Magdalena, ni muogeleaji mzuri, hajapendelewa, ” alisema Amina.
Sonia Tumiotto
Muogeleaji wa Tanzania Sonia Tumiotto (katikati) akiwa katika picha ya pamoja baada ya kushinda medali ya dhahabu katika mashindano ya Dubai. Sonia  alitwaa medali tatu katika mashindano hayo pia yaliandaliwa kwa ajili ya kutafuta tiketi za kufuzu Olimpiki Dubai.
Share on Google Plus

About Unknown

0 comments:

Post a Comment

Disqus Shortname

Comments System

Disqus Shortname

Comments system