Comments


Azam yaing'oa Yanga SC kileleni

Nahodha John Bocco 'Adebayor'


Mabao mawili ya nahodha John Bocco 'Adebayor' na mengine mawili ya washambuliaji wa kimataifa Didier Kavumbagu na Kipre Tchetche yalitosha kuipa Azam FC ushindi wa 4-2 dhidi ya JKT Ruvu kwenye Uwanja wa Karume jijini Dar es Salaam jana.
Matokeo ya mechi hiyo ya raundi ya tisa ya Ligi Kuu Tanzania Bara iliyochezeshwa na Mwamuzi Bora wa msimu uliopita, Israel Nkongo, yameifanya Azam kufikisha pointi 22, hivyo kuing'oa Yanga kileleni mwa msimamo kwa mara ya kwanza baada ya siku 47 (saa 1128) tangu Septemba 13 timu hiyo ya Jangwani ilipouanza msimu kwa kushinda 2-0 dhidi ya Coastal Union.
Kavumbagu aliyekuwa katika ubora wake jana akipika mabao mawili, alifungua karamu ya mabao ya Azam jana akimalizia kiufundi krosi ya beki wa kulia Shomari Kapombe dakika ya nne ya mchezo kabla ya Bocco kufunga la pili dakika mbili baadaye.
Dakika moja baada ya nusu saa ya mchezo, Najim Magulu aliwafungia wenyeji akimalizia mpira uliowababatiza mabeki wa Azam baada ya faulo kali iliyopigwa na mshambuliaji Saad Kipanga na kuzifanya timu hizo kwenda mapumzikoni matokeo yakiwa 1-2.
Bocco alifunga bao la tatu kwa penalti iliyoamuliwa na refa Nkongo baada ya Kapombe kukwatuliwa na Paul Mhidze ndani ya boski dakika ya 64, lakini dakika tano baadaye Emmanuel Pius akajibu mapigo kwa kuipatia JKT Ruvu goli la pili.
Baada ya bao hilo, Kocha wa Azam FC alifanya mabadiliko kwa kuwaingiza Erasto Nyoni kwa ajili ya kuongeza ulinzi na Tchetche ili kuongeza makali ya safu ya ushambuliaji, mabadiliko ambayo yalijibu baada ya Muivory Coast huyo kufunga bao la nne akikokota mpira hadi ndani ya boksi kabla ya kupiga shuti kali lililompita kipa Shaban Dihile.
Katika mechi nyingine ya ligi hiyo jana, Tanzania Prisons walishinda 1-0 nyumbani dhidi ya African Sports ya Tanga kwenye Uwanja wa Sokoine jijini Mbeya, shukrani kwa bao la tuta lililopigwa na 'muuaji' wa Simba, Mohamed Mkopi na kuiwezesha timu yake kupanda hadi nafasi ya sita.
Share on Google Plus

About Unknown

0 comments:

Post a Comment

Disqus Shortname

Comments System

Disqus Shortname

Comments system