Wafanyabiashara wanaotoa huduma katika masoko wametakiwa kudumisha utaratibu wa kufanya usafi katika maeneo yao ya biashara pasipo kushurutishwa ili kulinda afya za watumiaji wa bidhaa wanazouza, ikiwa ni jitihada za kupambana na ugonjwa wa kipindupindu.
Pia imeelezwa kuwa maeneo mengi ya masoko usafi wake hauridhishi kutokana na tabia ya baadhi ya wafanyabiashara kutokushiriki kikamilifu katika kufanya usafi.
wafanyabiashara wa soko kuu lililopo katikati ya jiji la Arusha pamoja na wananchi na watumishi kutoka idara mbalimbali za serikali wamewajibika kufanya usafi ikiwa ni jitihada za kupambana na maradhi yatokanayo na uchafu.
Baadhi ya wafanyabiashara wa soko hilo wamesema bado inahitajika elimu ya kutosha ili wananchi wawe na uelewa katika kusafisha na kutunza mazingira.
Kwa upande wake mkuu wa wilaya ya Arusha Fadhili Nkurlu ambaye naye ameshiriki kufanya usafi amewataka wafanyabiashara na wananchi wote kwa ujumla kushiriki kikamilifu kufanya usafi ikiwa ni jitihada za kukabiliana na magonjwa ya mlipuko ukiwemo ugonjwa wa kipindupindu.
Licha ya usafi unaotakiwa kufanyika kila siku serikali ya mkoa Arusha imetenga kila jumamosi ya kwanza ya kila mwezi kuwa ni siku ya kushiriki kwa pamoja kufanya usafi katika viunga vya jijini hapa.
0 comments:
Post a Comment